MAKALA



 UMUHIMU WA SWALA NA NAFASI YAKE KATIKA UISLAMU


A: HUKUMU YA SWALA KWA MUJIBU WA QUR-ANI NA SUNNAH
Ewe ndugu yangu mpenzi; hebu kwa msaada wa Mwenyezi Mungu Mtukufu tuzianze nasaha zetu kwa kumuomba Mola wetu Mtukufu atuwafikshe na kutuongoza katika kuijua haki, kuikubali na ksha kuifuata-Aamiyn Baada ya dua hiyo, hebu sasa tutazame kwa pamoja natujiulize nini hukumu ya ibada ya swala ndipo tutafahamu ni ipi nafasi na hukumu ya mtu asiye swali .

Ndugu yangu mpenzi, elewa na ufahamu kwamba swali katika sheria ni FARDH yaani WAJIBU. Haya ni kwa mujibu wa aya chungu mzima za Qur-ani Tukufu. Hebu tusitafakari kwa pamoja aya hizi zifuatazo

"…BASI SIMAMISHENI SWALA, KWANI HAKIKA SWALA. IMEKUWA KWA WAUMINI NI FARDHI ILIYOWEKEWA WAKATI MAALUM" [4:103]
Ukizingatia aya hii utakuta inaeleza kwa ufumbulizo na uwazi kabisa kwamba swali ni FARDHI, tenasi fardhi tu bali ni fardhi iliyowekewa wakati maalum na Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa waja wake waumini kauli ya Mola karim Aliposema: "… HAKIKA SWALAKWA WAUMINI NI FARDHI ILIYOWEKEWA WAKATI MAALUM " ni ishara na dalili bayana kwamba swala ndio kielelezo kikubwa cha Imani ya mja. Kwa maneno mengine tunaweza kusema kuwa hana Imani, mtu asiyeswali. Ikiwa mtu hana Imani , vipi unamtazamia kuwa na dini? Hii ndio maana Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie akasema: Mkimuona mtu aizoya Msikiti basi mshudieni kuwa yuna Imani kauli hii ya Bwana Mtume inazidi kutuonyesha ukweli usio pingika kwamba swala ndio nembo na kielelezo kikubwa cha Imani ya mja. Hebu tuitafakari na aya hii:- "HIFADHINI (angalieni sana) SWALA (zote kuziswali) NA (khasa) ILE SWALA YA KATI NA KATI "[2:238]

Tukilizingatia neno la mwanzo lilotumika katika aya (HIFADHINI) tukaliweka katika sarufi ya kiarabu (Arabic Grammar), tutaambiwa na watu wa fani ya lugha kuwa neno hili ni tendo la amri. Kwa hivyo basi neno hili (HIFADHINI) inbamaanisha kuwa suala la kuhifadhi swala ni amri itokayo kwa Mwenyezi Mungu kuja kwa waja wake na wala sio ombi. 

Sasa kama tunakubaliana na ukweli huu ulio dhahiri kuwa swala ni amri ya Mola amuamrisha mja wake, je! Huoni kwamba kuacha swala ni kupinga na kuivunja amri ya Muumba wako? Avunjaye na kupinga amri ya Bwana wake hufanywaje na Bwana wake, hasa ukizingatia kwamba siku zote amri hutoka kwa Mkubwa aliye kuja juu kwa mdogo aliye chini kama ambavyo ombi hutoka kwa aliye chini kuja kwa aliye juu. 

Hebu jaribu kuwa mkweli, mwanao au mkeo akivunja amri yako, unakuwaje na unchukua hatua gani? Ukiukir ukweli huu ndipo utaiona nafasi yako mbele ya Mola wako wewe usiyetaka kumsujudia Mola wako.

Naam, tumetangulia kusema huko nyuma kwamba swala ni FARDHI /WAJIBU, hebu sasa tulitazame neno WAJIBU limeaanishwa vipi na sheria ili uione nafasi yako wewe usiyeswali. Wataalamu wa fani ya fiq-hi wamelianisha neno wajibukwa kusema (WAJIBU/FARDHI ni lile jambo ambalo Allah ameliwajibisha juu yetu, hulipwa mtu aliye baleghe (mtu mzima),mwenye akili timamu kwa kulitenda/kulitekeleza (hilo la wajibu)na huaadhibiwa kwa kuwacha kulitenda, kama vile swala, funga na kuwatii wazazi). Hili ndilo ainisho (definition) sahali la WAJIBU, hebu sasa lichukuwe aanisho hili uliambatishe na swala, unafahamu nini? Ikiwa wewe ni mkweli, uliokulazimu kwa amri ya Mola Muumba wako na kwamba ukiswali utakuwa umeikubali na kuipokea kuitekeleza amri ya Mola wako kwa maslahi na faida ya nafsi yako, hivyo utalipwa thawabu ambaazo ndizo "Dollar" za kuinunulia akhera. Kinyume chake ni kwamba kama hukuswali utakuwa umeipuzana na kuivunja amri ya Molawako kwa maangamivu na khasara ya nafsi yako mwenyewe, kwa hivyo utaaadhibiwa kwanza hapa hapa duniani, kaburini na kesho akhera kama lilivyothibiti hilo katika hadithi ya Mtume –Rehema na Amani zimshukie. Tusome kwa mazingatio: "… NA BILA SHAKA ADHABU YA AKHERA NI KALI ZAIDI NA IENDELEAYO SANA"[20:127]
"ANAYEFANYA MEMA ANAJIFANYIA (mwenye) NAFSI YAKE, NA MWENYE KUTENDA UBAYA NI JUU (ya nafsi) YAKE NAMOLA WAKO SI DHALIMU KWA WAJA WAKE."[41:46]

B: NAFASI YA SWALA KATIKA UIISLAM
Katka kuonyesha umuhimu na nafasi ya swala,Bwana Mtume- Rehema na Amani zimshukie –ameijaalia swala kuwa inashika nafasi ya pili katika nguzo tano za uislam "uislamu umejengwa juu ya nguzo tano: kushuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa ila Allah na Muhammad ni Mtume wa Allah, kusimamisha swala, kutoazakah, kufunga ramadhani na kuhiji Makkah-Mukaram" Bukhaariy.

Ukiitafakari hadithi hii utaona ya kwamba Mtume –Rehema na Amani zimshukie –anaumathihsha uislamu na mfano wa jengo kubwa, imara na madhubuti lililojengwa juu ya nguzo tano. Hapana hata mmoja awezaye kupinga kwamba kuna jengo linaloweza kusimama bila ya nguzo. Kama tunakiri ukweli huu, basi ni dhahiri kwamba hapana uislam pasipo na nguzo tano hizi na pasipo na nguzo na uislam pana kufru tu si vinginevyo. 

Eeh Mola wetu tukinge na ukafiri kwa kutujulia kuisimamisha swala maisha yetu yote Aamiyn. Inakupasa uelewe ewe nduguyangu mpenzi muislam kwamba swala ndio nguzo tukufu kabisa ya dini na nafasi na umuhimu wa swala katika uislamu ni kama vile ilivyo nafasi na umuhimu wa kichwa katika kiwiliwili. Basi kama ambavyo asivyokuwa na uhai mtu asiye na kichwandivyo ambavyo hana uislamumtu asiye na swala. Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie anatuasa kwa kutuambia : "Ye yote atakuyeicha swala kwa makusudi, bila ya shaka amekufuru" Twabraaniy.

Haya hebu jiulize ewe Ndugu yangu Muislamu na uihurumie nafsi yako, mtu aliyekufuru ana Uislamu ?! Fahamu ewe Ndugu yangu unayemuasi Mola wako kwa kuacha kuswali kwamba sala ndio nguzo ya dini hii, dini haipo bila ya nguzo hii. Haya yanathibitishwa na kauli ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – "Swala ndio nguzo ya dini, atakayeisimamisha, hakika ameisimamisha dini na atakayeiacha, bila ya shaka huyo ameivunja dini". Kwa mantiki hii, mtu atakayeihifadhi nguzo hii kwa kuswali katika nyakati zake maalumu na akatimiza sharti na nguzo zote hali kujinyenyekeza kwa Mola wake na huku akiamini kuwa ni wajibu wake kuswali, huyo ndiye atakayefaulu duniani na akhera. 

Tunasoma ndani ya Qur-ani Tukufu : "KWA YAKINI WAMEFAULU WAUMINI AMBAO WAO NI WANYENYEKEVU KATIKA SWALA ZAO" Al-Muuminun : 1-2. Kinyume chake yule atakayeipuuzia swala, akaacha kuswali, huyo ndiye mtu muovu aliyepata khasara duniani na akhera kwa sababu ya kuikhalifu amri ya Mola Muumba wake. Kwa mujibu wa kauli iliyotangulia ya Bwana Mtume, wewe usiotaka kuliweka paji lako la uso ardhini kumsujudia Mola wako umeichukua nyundo kubwa na nzito unaivunja na kuibomoa dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu. 

Dini ambayo amewatuma mitume wake wote, tangu Nabii Adam mpaka Mtume wa mwisho Muhammad – Rehema na Amani ziwashukie wote – kuja kuisimamisha katika katika ardhi hii. Je, mbomoa dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu si mgomvi wa Allah, na hivi mtu anaweza kugombana na Allah kisha akatazamia kupata salama ?! La hasha.

Ewe mpenzi ndugu yangu, elewa na ufahamu kwamba swala ndiyo ibada ya kwanza kabisa aliyoiwajibisha Mwenyezi Mungu kwa waja wake. Amesema Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie - : "Cha mwanzo alichokifaradhisha Allah kwa umati wangu ni swala tano, na cha mwanzo kinachorufaishwa (kinachopanda mbinguni) katika amali (matendo) yao ni swala tano, na cha mwanzo watakachoulizwa katika amali zao ni swala tano …." Ndugu yangu mpenzi usiotaka kumsujudia Mola wako aliyekuumba, haikutoshi hadithi hii kuona ni jinsi gani ibada ya swala ilivyopewa umuhimu wa kwanza katika Uislamu ?! Amali zako zote njema ni lazima zitanguliwe na swala tano ndipo zikubaliwe, kinyume na hivyo amali hizo hazina maana bali ni sawa sawa na mavumbi yapeperushwayo. 

Ushahidi wa haya ni kauli ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – "Cha mwanzo atakachokaguliwa/atakachohesabiwa mja siku ya kiyama ni swala, ikitengenea zimetengenea baki ya amali zake nyingine, ikifisidika (swala) zimefisidika (zimeharibika) baki ya amali zake nyingine"

Ndugu mpenzi muislamu, ukiyakiri maneno haya ya Bwana Mtume yatakufikisha katika ukweli na hakika kwamba swala ndio ibada mama. Kadhalika ili kuonyesha utukufu wa ibada ya swala, utaikuta swala ndio ibada pekee aliyoitiwa Bwana Mtume na kukabidhiwa na Mola wake mbinguni. Ibada nyingine zote Bwana Mtume alikuwa akiletewa amri hapa hapa ardhini kupitia kwa malaika Jibril – Amani imshukie – Allah alimkuhutubu Mtume wake juu ya swala tano katika ule usiku wa Miraji pasina wasita wa Jibril. Amesema Anas – Allah amridhie – Imefaradhishwa swala kwa Mtume – Rehema na Amani zimshukie – usiku aliopelekwa mbinguni swala khamsini, kisha zikapunguzwa mpaka zikawa tano, kisha (Mtume) akaitwa ewe Muhammad ! Hakika maneno yangu hayabadilishwi na utapata wewe katika swala tano hizo ujira wa swala khamsini"

Ndugu yangu muislamu, hebu yatafakari kwa makini maneno ya Mtume wako, utauona utukufu wa ibada ya swala. Ni kwa ajili hiyo ndio tunaona Allah anatuamrisha kuhifadhi na kudumisha swala na muislamu amewajibikiwa kuitekeleza swala muda wa kudumu roho yake katika kiwiliwili chake. 

Akiwa mzima wa afya njema au mgonjwa asojiweza kitandani kwa sharti ya kuwa na fahamu za kujua alitendalo. Awapo vitani au katika hali ya amani, akiwa safarini au la, swala imemlazimu tu. Mwanamume na mwanamke wote ni sawa katika amri hii ya swala, ila mwanamke hatoswali akiwa katika hali ya hedhi au nifasi. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kuamrisha swala "HIFADHINI (angalieni sana) SWALA (zote kuziswali) NA (khasa) ILE SWALA YA KATI NA KATI NA SIMAMENI KWA UNYENYEKEVU KATIKA KUMUABUDU ALLAH NA MKIWA KHOFU ( mmo vitani, basi swalini) HALI YA KUWA MNAKWENDA KWA MIGUU AU MMEPANDA (wanyama) NA MTAKAPOKUWA KATIKA AMANI BASI MKUMBUKENI ALLAH (swalini) KAMA ALIVYOKUFUNZENI YALE MLIYOKUWA HAMYAJUI" [2:238-239]
Ndugu yangu mpenzi, utabainikiwa kutokana na aya hii kwamba muislamu hana udhuru hata chembe unaomuhalalishia kuacha swala. Hivyo basi muislamu atakayeitekeleza swala kama itakikanavyo, swala hiyo itakuwa ni hoja (wakili wa kumtetea) itakayomuokoa siku ya Kiyama, si hivyo tu bali itakuwa ni nuru itakayomuangazia na kumuongoza katika siku hiyo ngumu na nzito kama ambavyo itakovyokuwa ni sababu ya kufutiwa madhambi yake.
Imepokelewa kutoka kwa Sayyidna Uthman – Allah amuwie Radhi – amesema : nimemsikia Mtume – Rehema na Amani zimshukie – akisema : "Hatawadhi mtu udhu wake vizuri kisha akaswali ila Allah humsamehe mtu huyo madhambi yaliyo baina ya swala hii na swala ijayo". 

Basi ni kheri na furaha iliyoje kwa yule aliyeitekeleza swala kwa ukamilifu, ukamilifu na unyenyekevu mpaka anamaliza muda wake wa kuishi hapa duniani (anakufa). Eh! Ole wake, tena ole wake na majuto yake yule aliyefanya kibri, akaacha kuitekeleza swala hata akaondoka duniani bila ya kumsujudia Mola wake.
Hebu itegee sikio la usikivu kauli hii tukufu ya Allah asema nini juu ya watu hawa : "(Na wawalete) HIYO SIKU KUTAKAYOKUWA NA MATESO MAKALI NA WATAITWA KUSUJUDU LAKINI HAWATAWEZA. MACHO YAO YATAINAMIA CHINI; UNYONGE UTAWAFUNIKA NA HAKIKA WALIKUWA WAKIITWA KUSUJUDU WALIPOKUWA SALAMA (na walikataa)" [68:42-43].
Watu wa peponi watawauliza watu wa motoni : "NI KIPI KILICHOKUPELEKENI MOTONI ? WASEME : HATUKUWA MIONGONI MWA WALIOKUWA WAKISWALI. HATUKUWA TUKILISHA MASIKINI. NA TULIKUWA TUKIZAMA (katika maasia) PAMOJA NA WALIOKUWA WAKIZAMA" [74:42-45]. Khasara na maangamivu yaliyoje, leo utawaona baadhi ya waislamu hawaswali na hoja yao kubwa shughuli nyingi hawana nafasi, wametingwa na kazi na wengine huthubutu hata kusema kwa kinywa kipana kabisa kwani ni lazima kuswali, kama ninafanya mema mengine haitoshi ?! Hebu itegee sikio kauli hii ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie - : "Yeyote yule atakayeihifadhi swala, iatkuwa (swala hiyo) ni nuru, hoja na uokovu kwa mtu huyo siku ya Kiyama, na yeyote yule asiyeihifadhi swala, haitokuwa (swala) ni nuru, hoja na uokovu kwa mtu huyo, bali atakuwa (motoni) siku ya Kiyama pamoja na akina Qaarun, Fir-aun, Haaman na Ubayyi bin Khalaf".
Fahamu ewe ndugu yangu muislamu, swala ina nafasi na utukufu wa pekee katika Uislamu ndio maana tunamkuta Bwana Mtume mara nyingi anatuhimiza swala na swala ndio ulikuwa wasia wake wa mwisho wakati anaondoka duniani : "Ninakuhimizeni na kukuusieni swala pamoja na wamilikiwa wa mikono yenu ya kuume".
C. KHATARI YA KUACHA SWALA
Ndugu yangu Muislamu, bila shaka unatambua au umewahi kusikia kwamba Allah aliwaamrisha malaika pamoja na Ibliis wamsujudie baba yetu Nabii Adam – Amani imshukie – hali ya kumuamkia.
Iblisi kwa ushupavu na kibri alichokuwa nacho alikataa kuitii na kuitekeleza amri ya Mola wake. Ni kwa sababu hii tu Allah akamfukuza Iblis na kumtoa huko alikokuwa pamoja na Malaika na akamlaani mpaka siku ya kiyama, na kesho akhera ataingia motoni. 

Tusome kwa mazingatio : "(na wakumbushe watu khabari hii) TULIPOWAAMBIA MALAIKA MSUJUDIENI ADAM ( yaani mwadhimisheni kwa ile elimu yake aliyopewa) WAKAMSUJUDIA WOTE ISIPOKUWA IBLIS, AKAKATAA NA AKAJIVUNA NA (toke hapo) ALIKUWA KATIKA MAKAFIRI (ila tu alichanganyika tu na malaika)" [2:34].

Basi wewe ndugu yangu mpenzi usiotaka kuswali, hujioni kuwa wewe ni mbaya zaidi kuliko Iblis ?! Iblis alikataa kumsujudia Nabii Adam, wewe leo unakataa kumsujudia aliyemuumba Nabii Adam.
Iblis alikataa kusujudu mara moja tu, wewe leo unakataa kusujudu mara thelathini na nne (34) kila siku, mara 238 kila wiki, mara 1020 kila mwezi, mara 12,104 kwa mwaka, mara ….. katika umri wako, jaza mwenyewe. Iblis alikataa kusujudu sijida ya heshima kwa Nabii Adam, wewe unakataa kusujudu sijida ya ibada kwa Mola Muumba wako.
Hebu angalia tena adhabu aliyopewa Iblis kwa kuacha sijida moja tu alilaaniwa na kutolewa peponi na huku akisubiriwa kuliongoza kundi la watu wa motoni kuingia motoni.
Hii inamaanisha mwenye kuacha sijida 34 kila siku anastahiki kupata adhabu kali zaidi ya ile aliyopewa Iblis mlaaniwa, sikwambii asioswali juma moja au zaidi. Ndugu yangu usioswali unatarajia nini ikiwa hali ni hiyo ?! Unaona uzito gani kumsujudia Mola wako ?! Aletwe Mtume mwingine ndio utasikia na kutii ?! Hebu ihurumie nafsi yako, huiwezi adhabu ya Mola wako.
Ndugu yangu umepewa neema ya akili, ishukuru neema hiyo kwa kuzingatia uambiwayo, umepewa masikio ili usikie, isikie haki na kuifuata, usijitie upofu na uziwi wa bure ukajuta na kuangamia.
Zinduka, usiingie katika kauli ya Allah isemayo : "NA BILA SHAKA TUMEWAUMBIA MOTO WA JAHANAMU WENGI KATIKA MAJINI NA WANADAMU (kwa sababu hii): NYOYO WANAZO LAKINI HAWAFAHAMU KWAZO, NA MACHI WANAYO LAKINI HAWAONI KWAYO, NA MASIKIO WANAYO LAKINI HAWASIKII KWAYO. HAO NI KAMA WANYAMA, BALI WAO NI WAPOTOFU ZAIDI. HAO NDIO WALIOGHAFILIKA" [7:179].
Tahadhari ewe ndugu yangu, usiwe na sifa hizi zilizotajwa, kwani hizi ni sifa za watu wabaya, watu wa motoni. Tumuombe Mola wetu Mtukufu asitujaalie kuwa miongoni mwa watu wa motoni, wasiotaka kumsujudia – Amin. 




  
RUSHWA:HATARI NA ATHARI ZAKE


 RUSHWA:HATARI NA ATHARI ZAKE

Msemo "Rushwa ni adui wa haki", kelele zinapopigwa ulimwenguni kote na wanasiasa, viongozi na serikali na wale wa dini dhidi ya rushwa. Haya yote ni ishara na dalili wazi juu na namna jamii inavyoathirika na kukerwa na mdudu mbaya huyu, rushwa. Rushwa ni mdudu mwenye athari mbaya sana kwa jamii, mdudu anayeua bila huruma haki za kimsingi na za kijamii.
Mwenyezi Mungu Mtukufu anatuasa:

"WALA MSILIANE MALI ZENU KWA BATILI NA KUZIPELEKA KWA MAHAKIMU ILI MPATE KULA SEHEMU YA MALI YA WATU KWA DHAMBI NA HALI MNAJUA" [2:188]. Amesema swahaba wa Mtume-Ibn Abbas-Allah amuwiye radhi-katika kuitafasiri aya hii: Katazo hili linamuhusu mtu mwenye kumiliki mali bila ya uhalali wowote, kisha akamuendea hakimu kutaka kupata uhalali wa kumiliki na ilhali anajua fika kuwa haki si yake. Huyo aelewe kuwa anapata dhambi na anachokila ni haramu.

Aya inafahamisha kuwa hukumu ya huyu hakimu kumuhalalishia dhalimu na kumpa haki asiyoistahiki haibadilishi chochote hakika na ukweli. Hakika itabakia pale pale mbele ya Mwenyezi Mungu kuwa mali ile si haki yake na ukweli ni kuwa mali itabakia kuwa ni haramu inayompatia dhambi za uovu wake huo.
Kwa mantiki hii, hakimu muhalalishaji wa haramu hali anajua na dhalimu muhalalishiwa haramu hali nafsi yake inakiri kuwa haramu wawili hawa watashirikiana katika dhambi za uovu huu.

Mwenyezi Mungu anatukataza na kutuonya katika aya hii kula au kuchukua mali ya mtu kwa njia ya batili yaani kwa njia isiyo ya halali. Kula mali ya mtu katika njia ya batili ni pamoja na kupokonya, kupora,kudhulumu,kupokea rushwa na kadhalika. Kwa nini Mwenyezi Mungu amesema:" WALA MSILIANE MALI ZENU", akatumia neno KULA badala ya KUCHUKUA. Neno KULA limetumika kwa kuwa ndio makusudi na lengo kuu la kuchukua/kupata mali. Mporaji anapopora ili ale, dhalimu anadhulumu apate kula, mpokea rushwa anapokea pia kwa ajili ya Tumbo. 

Hili ndilo lengo la kwanza, kisha ndio hufuatia mengine kama vile kuvaa,kujenga,kununua gari,shamba na kadhalika. Ndio maana watu husikika wakisema (Fulani anakula mali za watu) wakiimanisha: Anachukua mali za watu bila ya uhalali,kwa njia batili.

Mwenyezi Mungu amewaumba wanadamu na akawapangia na kuwawekea sheria zitakazoyatawala maisha yao katika ulimwengu huu wa muda,ili waishi kwa amani,salama na utulivu. Mwenye nguvu asimdhulumu mnyonge wala mkubwa asimuonee mdogo. 

Basi mfanyakazi anayepokea rushwa kwa ajili ya kutoa huduma,huyu anaivunja misingi ya amani katika jamii, anavuruga nidhamu/utaratibu wa sheria. Huyu mbali ya kuwa ana hatia mbele ya mahakama adilifu ya Mwenyezi Mungu pia anaikosea jamii nzima kwa kuwa anapokea ujira kwa kuivunja amani. 

Mtoaji wa rushwa pia haiepuki hatia kwa kuwa kutoa anatoa ujira kufisidi/kuharibu uadilifu. Mali anayoipokea mlaji rushwa ni moto na ataadhibiwa kwa uchukuaji wa mali hiyo adhabu kali kabisa, kwa sababu ya kuvunja kwake sheria ambayo misingi yake mikuu ni uadilifu na amani. Hebu uone ubaya na athari ya rushwa kwa jamii kupitia mifano hali ifuatayo:

Serikali/Shirika la umma limetangaza nafasi za kazi.
Wananchi wenye sifa zinazotakiwa wakajitokeza kujaza nafasi hizo. Mtu aliyekabidhiwa na umma dhamana ya kuhoji watu hawa na hatimaye kuwaajiri wanaostahiki.
Huyu anayapiga teke maadili na muongozo wa kazi yake,badala ya kuwachagua watu kwa sifa husika, yeye anawachagua watu kwa vigezo vya udugu, na kwa kupewa rushwa.
Natija ya uchaguzi huu ni kuwapa ajira watu wasiostahili, jambo ambalo litasababisha utendaji mbovu usio na ufanisi, utendaji utakaopelekea kufilisika na hatimaye kufa kwa shirika ambalo ni mali ya umma. Uharibifu wa mtu mmoja huyu mwenye maradhi hatari ya rushwa unasababisha kuathirika kwa jamii nzima ni kwa sababu hii ndiyo Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie –akaikemea vikali rushwa aliposema "Mtoaji na mpokeaaji rushwa (wataingia ) motoni". At-twabraaniy.

Utamuona leo daktari anayetupilia mbali maadili ya kazi yake, anavua utu wake na kuuvaa unyama. Anamuacha mgonjwa kufa mbele ya macho yake eti tu kwa sababu hakupewa chai (rushwa). 

Huu ndio ukweli na sote tunishuhudia hali hii kila leo. Mdudu rushwa ameiondosha kabisa huruma ndani ya moyo wa daktari kiasi cha kuwa maisha ya binadamu mwenziwe hayana thamani kama hakupewa rushwa.
Ni kutokana na athari hii mbaya ya rushwa ndio Bwana Mtume –Allah amshushie Rehema na Amani –akasema "Allah amemlaani mtoaji na mpokeaji rushwa na mkaa kati yao". Ahmad

Hebu tuangalie hakimu anayepewa dhamana ya kusimamia haki. Huyu kwa sababu ya kitu kidogo alichopewa (rushwa) anampa haki mtu asiyestahiki na kumnyima mwenye haki au anamfunga mtu kwa dhuluma kwa sababu tu kuna mtu anataka kumkomoa au anamuachia huru mtuhumiwa aliyetiwa hatiani na sheria kwa ajili ya kupewa rushwa.

Hizi ni baadhi tu za athari nyingi za rushwa kwa jamii. Rushwa ikienea katika jamii husika, tabia za watu zitaharibika,utu na heshima vitatoweka na badala yake unyama,chuki na uadui ndivyo vitaitawala jamii hiyo kama tulivyoona katika mifano yetu hai. Mla rushwa ni mtu mbaya na hatari sana katika jamii.
Huyu hana utu, hana haya wala huruma na ndio maana Bwana Mtume hakumuonea haya kumshushia laana za Mwenyezi Mungu. 

Ewe ndugu yangu uliyelemazwa na maradhi ya rushwa hebu jiulize na kisha ujihurumie. Jee, unaweza kuibeba laana ya Mola wako? Kulaaniwa na Mwenyezi Mungu maana yake ni kutengwa na Rehema za Mola duniani na akhera , Je, utasalimika ikiwa hukupata rehema za Mola wako? Kutokupata rehema kunaamaanisha kupata ghadhabu je ndugu yangu unao ubavu wa kuhimili ghadhabu za Mola wako. 

Ikemee nafsi yako, acha kuanzia leo tabia mbaya ya kupenda na kupokea rushwa kwa huduma ambayo unawajibika kuitoa huku ukiitafakari kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:-

"ANAYEFANYA MEMA ANAJIFANYIA (mwenyewe) NAFSI YAKE,NA MWENYE KUTENDA UBAYA NI JUU (ya nafsi)YAKE (vilevile) NA MOLA WAKO SI DHALIMU (hata kidogo) KWA WAJA (wake). [41:46]
Chagua sasa,kuendelea kula rushwa kwa khasara na maangamivu ya nafsi yako mwenyewe au kuacha kula rushwa kwa faida na maslahi ya nafsi yako. Kumbuka "Rushwa ni adui wa haki" na mla rushwa ni "Adui wa Mungu, Mtume na watu wote"


  

NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII YA KIISLAMU



Nabii Muhammad – Rehema na Amani zimshukie – alipotumwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu kuja ulimwenguni kuuhusisha Uislamu ulioasisiwa na Mitume waliomtangulia, alimkuta mwanamke akiishi chini ya mazingira na kivuli cha ukandamizaji. Katika ulimwengu ule, mwanamke hakuwa na haki yeyote ile katika jamii yake bali alionekana kama ni bidhaa inayoweza kuuzwa wakati wowote.
Mwanamke alichukuliwa kama ni chombo cha kumstarehesha na kukidhi matamanio ya kimwili ya mwanamume. 

Mwanamke alihesabika kuwa ni chombo cha uzalishaji na hakuwa na uchaguzi/uhuru wa kupanga na kuamua. Haya kwa mukhtasari ndiyo mazingira ambayo Uislamu ulimkuta mwanamke akiishi chini ya anga lake. 

Mwenyezi Mungu kupitia mfumo sahihi wa maisha (Uislamu) ambao dhamana ya uongozi wake alimpa Nabii Muhammad – Rehema na Amani zimshukie – akamuondolea mwanamke unyonge, udhalili, dhulma, uonevu na unyanyasaji ule. Uislamu ukamjengea mwanamke mazingira bora, kanuni na sheria ambazo zitamuhakikishia uhuru, usalama, amani, haki na usawa katika jamii yake. 

Uislamu ukamtayarishia mwanamke anga zuri, chini ya anga hilo ataishi huku akijihisi kuwa ni binadamu kamili, mwenye haki sawa kama mwanamume na ukamdhaminia kupata haki zote kama binadamu bila ya kuhitajia upendeleo maalum kama tusikiavyo istilahi hii ikipigiwa kelele ulimwenguni kote bila ya utekelezaji wowote. 

Uislamu ukamuondoshea mwanamke tuhuma ya kumpotosha Baba yetu Adam – amani iwashukie wote – peponi na kuwa yeye (mwanamke) ndiye asili na chanzo cha uovu wote huu utendekao ulimwenguni. Uislamu ukabainisha kwamba ni shetani mlaaniwa ndiye aliyewapoteza Nabii Adam na mama yetu Hawaa, kama tunavyosoma katika kitabu cha Uislamu "(Lakini) SHETANI (yule Iblis adui yao) ALIWATELEZESHA WOTE WAWILI (wakakhalifu amri ile, wakala katika mti huo waliokatazwa) NA AKAWATOA KATIKA ILE (hali) WALIYOKUWA NAYO …[2:36].

Uislamu unakiri na kutangaza wazi kuwa watu wote bila ya kujali rangi au hali zao kimaisha wameumbwa kutokana na nafsi moja tu. Tusome, tuzingatie na tukubali : "ENYI WATU ! MCHENI MOLA WENU AMBAYE AMEKUUMBENI KATIKA NAFSI (asili) MOJA …." [4:1]
Huu ni usawa wa binadamu katika mfumo adilifu wa maisha (Uislamu). Chini ya kivuli cha mfumo huu, mwanamke na mwanamume wanaogelea pamoja katika bahari moja ya usawa wa haki zote za msingi za binadamu bila ya kubaliwa. Isitoshe ule utukufu ambao Mwenyezi Mungu Mtukufu aliompa mwanadamu katika kauli yake : "NA HAKIKA TUMEWATUKUZA WANADAMU …" [17:70]. 

Huu ni utukufu aliozawadiwa mwanadamu yoyote bila ya kuangalia ni mwanamume au mwanamke, wote wanashirikiana kwa usawa katika utukufu huu. Qur-ani Tukufu inapomzungumzia mtu au wanadamu, basi huwa inamkusudia mwanamume pamoja na mwanamke. Ama inapotaka kumtaja mwanamume au mwanamke peke yake bila ya kumhusisha mwenzake basi hutumia istilahi "wanamume" au "wanawake".

Mtume – Rehema na Amani zimshukie – anazidi kuudhihirisha ulimwengu nafasi aliyonayo mwanamke katika mfumo huu sahihi wa maisha (Uislamu). 

Anatuonyesha uhusiano uliopo baina ya mwanamume na mwanamke katika kauli yake: "Wanawake ni ndugu baba mmoja, mama mmoja na wanamume, wanayo haki kwa sheria (kufanyiwa na wanamume) kama ile haki iliyo juu yao kuwafanyia wanamume" Abu Dawoud. Istilahi ya ndugu baba mmoja, mama mmoja aliyoitumia Bwana Mtume inatoa sura kamili ya usawa baina ya mwanamke na mwanamume.

Kwa jicho la mfumo kamili huu wa maisha (Uislamu) wanamume na wanawake kiasili ni sawa sawa bila tofauti yeyote mbele ya Mola wao. Ila tofauti na ubora utajitokeza katika amali njema anazozifanya kila mmoja wao, ni dhahiri kuwa mzuri na mwingi wa amali njema hawezi kulingana sawa na mchache wa amali njema bila ya kuangalia ni mwanamume au mwanamke, hii ndio mojawapo wa misingi na kanuni za Uislamu. 

Tusome kwa mazingatio na kutafakari : "WAFANYAJI MEMA, WANAMUME AU WANAWAKE, HALI YA KUWA NI WAISLAMU, TUTAWAHUISHA MAISHA MEMA NA TUTAWAPA UJIRA WAO (Akhera) MKUBWA KABISA KWA SABABU YA YALE MEMA WALIYOKUWA WAKIYATENDA" [16:97]. 

Uislamu unazidi kumthibitishia na kumuhakikishia mwanamke nafasi ya usawa kwa kumpa fursa sawa ya kukubaliwa na kujibiwa dua sawa sawa/sambamba na mwanamume bila ya kupoteza amali zake njema. Hili linathibitishwa na Qur-ani Tukufu : "MOLA WAO AKAWAKUBALIA (maombi yao kwa kusema) HAKIKA MIMI SITAPOTEZA JUHUDI (amali) YA MWANAMUME AU MWANAMKE (kwani nyinyi) NI NYINYI KWA NYINYI …" [3:195].Muundo wa maelezo ya Qur-ani Tukufu NI NYINYI KWA NYINYI unatufahamisha kuwa kuna hali ya kutegemeana baina ya mwanamume na mwanamke na kwamba maisha ya kila mmoja wao hayakamiliki bila ya kushirikiana na mwenziwe.
Uislamu unauthamini mchango wa mwanamke katika jamii, ndio maana ukampa nafasi na haki sawa ya kushiriki katika vitakatifu vya kidini "Jihadi" sambamba na mwanamume. 

Katika medani ya vita kuna watakaokufa mashahidi, kuna majeruhi, wapiganaji ni wanadamu wanahitaji huduma ya maji na chakula. Nani atakayetoa huduma hizi ili kuipa ushindi dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu ? Hapo ndipo unapoonekana umuhimu wa mchango wa mwanamke katika kuipigania dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu.
Ni kutokana na sababu hii na nyinginezo ndio tunamkuta Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alikuwa haendi katika vita vyovyote ila ataambatana na wanawake. 

Bibi Umayyah bint Qays ni mwanamke anayetajwa sana katika vitabu vya historia ya Uislamu kutokana na mchango wake mkubwa alioutoa katika vita vya Khaybar. Kwa kuuona na kuuthamini mchango wa bibi huyu, baada ya kumalizika vita hivi Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alimtunukia kidani alichokivaa maisha yake. 

Alipokurubia kufa aliusia azikwe pamoja na kidani chake – Allah amuwie radhi -. Mwanamke huyu na wale wote watakaomuiga wanaingia katika kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu : "LAKINI MTUME NA WALE WALIOAMINI PAMOJA WALIIPIGANIA (dini) KWA MALI ZAO NA NAFSI ZAO; NA HAO NDIO WATAKAOPATA KHERI; NA HAO NDIO WENYE KUFUZU (kufaulu) . ALLAH AMEWATENGENEZEA MABUSTANI YAPITAYO MITO MBELE YAKE, WAKAE HUMO. HUKO NDIKO KUFUZU KUKUBWA" [9:88-89]
Kadhalika Uislamu haukumuacha nyuma mwanamke katika uwanja wa elimu bali umemshirikisha kikamilifu sambamba na mwanamke. Hili linathibitishwa na kauli/agizo la Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie - : "Utafutaji/Kutafuta elimu ni fardhi ya lazima kabisa kwa kila muislamu mwanamume na muislamu mwanamke". Utaona kupitia agizo/kauli hii ya Bwana Mtume, Uislamu umewajibisha mwanamke apate elimu.
Hivi baada ya haki hizi za msingi alizopewa mwanamke wa Uislamu, haki ambazo zinalindwa na kusimamiwa na sheria madhubuti, kuna mtu muadilifu atakayefunua kinywa kipana na kudai kuwa eti Uislamu unamdhulumu na kumkandamiza mwanamke ?! Ndugu zanguni, ni lazima tukubali kuwa hapa kuna mambo mawili; Uislamu kama dini na mfumo sahihi wa maisha unaotawaliwa na sheria ya Allah na upande wa pili kuna wanaoitwa waislamu wanaitawaliwa na desturi/ada na mwenendo mbaya dhidi ya mwanamke. Kwa hivyo ni lazima tutofautishe baina ya vitu viwili hivi kama kweli tu waadilifu.
Kelele hizi na wimbo huu wa kunyanyaswa, kudhulumiwa na kunyimwa haki mwanamke zilizoenea leo ulimwenguni kote ni kelele zipigwazo na kambi za magharibi na mashariki.
Hawa hawana ushahidi wa kuyathibitisha madai yao haya bali kwa makusudi mazima wanataka kuipaka matope dini ya Mwenyezi Mungu Mtukufu; hawa ndio Mwenyezi Mungu anataumbia : "WANATAKA KUZIMA NURU YA ALLAH (Uislamu) KWA VINYWA VYAO; NA ALLAH ATAKAMILISHA NURU YAKE IJAPOKUWA WASHIRIKINA WATACHUKUWA" [61:8].
Tukifanya uchunguzi wa kiadilifu tutagundua kuwa ustaarabu wa kimagharibi ndio unaomnyima haki na kumdhulumu mwanamke. Ikiwa mwanamke anapoolewa huko katika ulimwengu wa kwanza (Ulaya) kwa watu walioendelea kama wanavyodai ananyimwa hata haki ya kuitwa kwa jina la baba yake mzazi bali ananasibishwa na familia ya mume aliyemuoa.
Kwa mfano mwanamke anayeitwa Vicky James akiolewa na Michael Brown anaitwa Mrs Vicky Brown.
Ikiwa mwanamke huyu hapati haki ya kuitwa kwa jina la baba yake aliyemzaa vipi unamtazamia kupata haki nyingine katika jamii hiyo ?! Katika Uislamu, mambo ni kinyume kabisa na hivyo. Wakeze Mtume, ambaye kwa mujibu wa imani ya kiislamu ndiye kiumbe bora kuliko wote hawakupata kuitwa mathalan Bibi Muhammad bin Abdillahi, bali waliitwa kwa majina ya baba zao, kama Bibi Aysha binti AbuBakri, Hafsa binti Umar, Zaynab binti Jahshi na kadhalika. Katika hali kama hii utawasikia na kuwaona watu wenye fikra lemavu waliorogwa na ukoloni mamboleo wakisema : Tunataka kuwa kama watu wa Magharibi. Huu ni udumavu wa fikra na mawazo.
Hivi kumvua nguo mwanamke na kumuacha uchi mbele ya kadamnasi ya watu katika kile kinachoitwa mashindano ya urembo, ndiko kumpa haki na uhuru mwanamke ? Huu ndio ustaarabu na maendeleo tunayotaka kuyaiga kutoka Magharibi ?! Je, kuja nyumbani kijana wa kiume na kumpiga busu mtoto wa kike mbele ya wazazi wake na kisha kumchukua kokote atakako na kumrudisha wakati autakao kwa madai ya uchumba na hili likapewa baraka zote za wazazi wa binti. Kijana akishamtia binti mimba amkimbie na kumuacha aubebe mzigo huo peke yake na kwenda kwenda kumtafuta kimwana mwingine na kustarehe naye na kuendeleza uchafu wake. Je, huu ndio usawa, haki na uhuru anaopewa mwanamke na ulimwengu wa magharibi na sisi tukataga kuuiga kibubusabubusa ? Haya si maendeleo bali maondoleo ya utu na maadili mema, na hizi ni tabia na silka za kinyama si za kibinadamu hata kidogo.
Huu ndio ukweli, tukikubali au kukataa. Uislamu haukuja kumdhulumu, kumuonea na kumkandamiza mwanamke, bali umekuja kumkomboa kutoka katika jahilia na kumpa haki zote anazostahiki kuzipata kama binadamu. 

Hebu tuhitimishe makala yetu haya kwa kuangalia mfano hai huu ambao unatoa sura/picha ya uhuru kamili ya kujieleza na kuchangia fikra aliopewa mwanamke chini ya mfumo sahihi wa maisha (Uislamu). Zama za ukhalifa(utawala) wa Sayyidna Umar – Allah amuwie radhi – wanawake walikuwa wakiwatoza wanamume mahari kubwa sana. Hali iliyopelekea baadhi ya wanamume wenye kipato duni kushindwa kuoa. 

Sayyidna Umar kama kiongozi mkuu wa dola ile ya kiislamu aliliona tatizo hili na kujiona kuwa anawajibika kulitafutia ufumbuzi wa haraka.
Akaamua kuitisha mkutano wa hadhara na kupiga marufuku utozaji mkubwa wa mahari na badala yake akaweka kiwango maalum cha mahari. Hapo ndipo aliposimama mwanamke mmoja na kusema : " Ewe Umar, ikiwa Mwenyezi Mungu mwenyewe ameturuhusu kuchukua mrundi wa mali (mali nyingi isiyo na idadi) vipi leo wewe unatuzuia na kutupiga marufuku kuchukua mali kidogo tu ? Hebu jaribu kufikiri huyu ni kiongozi wa dola, anaambiwa maneno hayo mbele ya watu na anayemwambia ni mwanamke, unafikiri alichukua hatua gani ? Sayyidna Umar aliuheshimu uhuru wa kujieleza na haki ya kusikilizwa ya mwanamke huyu. Akasalimu amri na kusema : Umar amekosea na mwanamke amepatia. Je, ni haki gani zaidi ya hizi tunataka apewe mwanamke ?! Hebu mchukue mwanamke huyu na umlete katika jamii yetu ya leo. 

Je, atathubutu kufungua kinywa chake na kumwambia kiongozi/mtawala maneno hayo ya kumkosoa mbele ya hadhira tena bila ya kuanza kwa kumuita mtukufu/mheshimiwa raisi, akamuita kwa jina lake tu, na kiongozi huyo akakiri mbele ya watu kuwa kweli kakosea ?! Hebu tuache chuki zetu na tujaribu kuwa waadilifu na wakweli ili tuweze kuiona haki kuwa ni haki na kuifuata na kuiona batili kuwa ni batili na tuiepuke.




KWA NINI UISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI

Haukuwa Uislamu ndiyo dini ya kwanza kuruhusu kuoa wake wengi na wala Uislamu haukuzua utaratibu huu. Bali Uislamu umekuwa ndiyo dini ya kwanza kuratibisha na kuyawekea utaratibu mzuri masuala ya ndoa. Isitoshe Uislamu ukaliwekea suala la kuoa wake wengi masharti madhubuti na magumu, ambayo Mume analazimika kuyazingatia kabla ya kuongeza mke/wake.

Suala la kuoa wake wengi halikuwa tu ni ada na desturi za waarabu zama za jahiliya, bali pia ilikuwa ni desturi ya mataifa mbalimbali kwa namna moja au nyengine, kama historia inavyokiri ukweli huu. Historia inaonyesha kuwa hata hapa kwetu Tanzania, watemi (machifu) wa makabila mbali mbali bali watu wa kawaida wenye mali walikuwa na wake wengi, huu ni ukweli usiopingika. Utaratibu huu wa kuoa wake wengi ulikuwemo pia katika vitabu vilivyotangulia Qur-ani Tukufu. Mna ndani ya Taurati maandiko na matukio yanayouthibitisha ukweli huu na wala hamna ndani ya Injili aya/maandiko yanayoharimisha kuoa wake wengi. Bali kuoa wake wengi kulizuiliwa na kanisa katika karne ya kati {karne ya 10-15 AD} na wakati mwingine waliruhusiwa na kanisa baadhi ya wafalme wakubwa kuoa wake wengi. Rejea vitabu vya historia ya kanisa.

Uislamu umeruhusu kuoa wake wengi kwa sharti

    isizidi idadi yao wake wanne
    Kufanya uadilifu baina yao.

Tunasoma ndani ya Qur-ani Tukufu juu ya ruhusa hii : "…. BASI OENI MNAOWAPENDA KATIKA WANAWAKE (maadam mtafanya uadilifu) WAWILI AU WATATU AU WANNE (tu). NA MKIOGOPA KUWA HAMWEZI KUFANYA UADILIFU, BASI (oeni) MMOJA TU, AU (wawekeni masuria) WALE AMBAO MIKONO YENU YA KUUME IMEWAMILIKI. KUFANYA HIVYO NDIKO KUTAPELEKEA KUTOFANYA UJEURI." [4:3]

Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alimwambia Ghaylan At-thaqafiy, ambaye alisilimu akiwa na wake kumi "Kaa na wanne (tu) miongoni mwao na waache (wataliki) waliosalia" At-tirmidhiy, An-nisaai na Ibn Maajah. Ni vema ikafahamika kwamba huyu Ghaylan alikuwa ndiye mtemi (mfalme) wa Twaif.

Suala hili la kuoa wake wengi ni suala lililofanywa na mwenyewe Bwana Mtume, maswahaba na waliokuja baada yao na ni suala ambalo umma mzima wa kiislamu umekongamana juu yake. Sheria hii inayomruhusu mwanamume kuoa zaidi ya mke mmoja ina maslahi na manufaa kwa wote wawili; mwanamume na mwanamke. Kwa upande wa mwanamume :

    Inawezekana kabisa mkewe akawa hamtoshelezei haja yake ya maumbile. Hili husababishwa na uwezo mkubwa wa mume katika tendo la ndoa na udhaifu wa mke. Mume hataki kumuacha mkewe, sasa ataitosheleza wapi kiu yake ? Hapo ndipo uislamu ukamruhusu kuoa mke mwingine na yule wa mwanzo kubakia pale pale. Lau uislamu usingemruhusu mume huyu kuongeza mke mwingine ni dhahiri kuwa ili kukidhi haja yake angefanya moja kati ya mawili. Ima angemtaliki huyu aliye naye, asiyekidhi haja na kuoa mwingine au angekuwa na nyumba ndogo (mwanamke wa pembeni/kimada)
    Kadhalika mwanamke anaweza kuwa tasa; hazai na mume anatamani kupata watoto, ambalo hili la kupata watoto ni mojawapo ya malengo na madhumuni ya ndoa. Lakini mume anampenda mkewe na kwa sababu moja au nyingine hataki kumuacha. Sasa huyu mume afanyeje ili aweze kupata watoto kuendeleza kizazi cha binadamu ? Akazae nje ya ndoa ? Hapana, hilo ni kosa. Hapa ndipo sheria ikaizingatia haki ya huyu mume kupata watoto na ikamruhusu kuoa mke mwingine ajaribu bahati yake. Huenda Mola wake akamruzuku watoto kwa mke huyu.

Haya ni baadhi tu ya maslahi ya sheria hii ya kuoa zaidi ya mke mmoja kwa upande wa mume. Hebu tuangalie mwanamke naye, ananufaika vipi na sheria hii :

    Inawezekana kabisa mke akapatwa na maradhi; yakamsababishia kushindwa kabisa kuitekeleza haki ya unyumba kwa mumewe. Maskini mke huyu mgonjwa, aende wapi na il-hali sasa katika kipindi kigumu cha ugonjwa ndio anahitajia zaidi huruma, mapenzi na liwazo la mumewe. Mumewe amtaliki ? La, hapana, sheria inambana mume kuwa katika mkataba wa ndoa alichukua ahadi kuishi naye katika raha/shida, uzima/ugonjwa, basi amuuguze mkewe na ili kukidhi haja zake za kimaumbile basi na aoe mke mwingine, Je hapo mwanamke hajanufaika?
    Kadhalika kama ambavyo binadamu anavyotofautiana katika sura, akili, tabia na kadhalika. Ni kama hivyo pia tunatofautiana katika uwezo/nguvu ya kujamiiana. Inaweza uwezo wa mume ukawa ni mkubwa sana kuliko mkewe, mume ni tembo na mke ni kondoo, vipi kondoo atahimili vishindo vya tembo ? Sasa, ili mke huyu asiichukie ndoa na hatimaye kukimbia, uislamu ukamruhusu mume kuongeza mke mwingine. Siku za zamu ya mke mwingine, huyu asiyehimili vishindo atapata kupumzika. Hebu tuwe wakweli, mwanamke huyu kanufaika au la?

Vile vile sheria hii ina maslahi makubwa kwa jamii. Hakuna jamii isiyokuwa na wajane na mayatima; ambao hawa wanataka wapate uangalizi na malezi. Nani basi atawalea wajane hawa waliofiwa na waume zao na hawa walioachwa na baba zao ? Hapo ndipo Uislamu ukampa ruhusa mwanaume ambaye tayari ana mke, kuongeza mke mwingine. Pengine huyu atakayemuoa ni huyo mjane, mwenye mayatima. Je hapo mwanamke huyu hajasitirika na wanawe ? Kwani huyu mume atakuwa anawajibika kumhudumia yeye na wanawe. Waswahili husema ukipenda boga penda na maua yake. Je, hapa jamii imenufaika au haikunufaika ?

Takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya wanawake duniani ni kubwa kuliko idadi ya wanaume, kadhalika idadi ya wanyama jike ni kubwa kuliko ya wanyama dume. Haya ni matokeo ya utafiti uliofanywa na taasisi mbali mbali ulimwenguni kote. Sasa itakuwa tunakubaliana na takwimu hizi na leo vita vimetapakaa duniani kote na wahanga (victims) wa vita hivi, wengi wao ni wanaume kwa kuwa wao ndio askari wanaopigana vita. Hebu tuchukulie/tukadirie kuwa uwiano wa wanaume na wanawake duniani 1:5 yaani mwanaume mmoja kwa wanawake watano. Sasa ikiwa kila mmoja akioa mke mmoja hawa waliobaki waende wapi, wakaolewe na nani ? Hawa pia ni binadamu, wanayo haki yao ya msingi ya kupenda na kupendwa katika jamii. Wanayo matakwa yao ya kimaumbile, wakakidhi wapi haja na hamu zao za kimaumbile ? Ni kwa kuzingatia hili ndio uislamu ukamruhusu mwanaume kuoa mke zaidi ya mke mmoja kwa sharti ya kuwa awe muadilifu baina yao.

Ni lazima tukubali kuwa kila sheria aliyotuwekea Mola wetu mtukufu ina faida,maslahi na manufaa kwetu sisi waja wake. Akiamrisha au kukataza ni kwa maslahi na faida yetu sisi wenyewe. Ni mamoja tumeyajua na kuyaona maslahi na faida za amri au katazo hilo au hapana. Kushindwa kwetu kuyajua maslahi na kuziona faida, hakuziondoshi faida na maslahi hayo na kuyafanya yasiwepo, bali yatabakia pale pale. Huu ndio ukweli usiopingika. Waislamu tumekuwa tukiwacha mafundisho ya dini yetu na kufuata mafundisho ya shetani yaliyopitia kwa wanaojiita wanamaendeleo. Leo matatizo yanayotukuta yanatokana na kuacha mafundisho ya Uislamu. Tukodolee macho wakati wa Mtume na masahaba na tuone nia zao katika kuoa wake wengi, jinsi mwanamke wa kiislamu alivyohifadhika, wajane wa vita pia nao hawakutupwa mkono, na Mtume –Rehema na Amani zimshukie – ndiye aliyeanza kuonyesha mfano. 

Je, tuna mfano mkubwa kuliko wa Mtume wakati Mwenyezi Mungu ndiye aliyetuamrisha tumfuate ? Tunafuata mkumbo wa maadui wa kiislamu unaodai haki za wanawake na kushikilia kuoa mke mmoja, pamoja na kuweka vimada, kumvunjia mwanamke heshima yake kwa kumvua nguo na kumtumia kwenye matangazo ya biashara, madansa, miss world na kadhalika. Leo mwanamke akiolewa ananyang’anywa hata jina la mzazi wake na kujulikana kwa jina la mumewe, Mrs fulani, sasa ni nani anayemtakia mema mwanamke, Mwenyezi Mungu aliyemuumba au wakazi wa dunia hii wakiongozwa na mwanaume ambaye yuko tayari kufanya lolote kutekeleza matashi ya nafsi yake ???



KWA NINI UISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI 

 KWA NINI UKWKWA NINI UISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI A NINI UISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI ISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI


 KWA NINI UISLAMU UMERUHUSU KUOA WAKE WENGI

No comments: