Thursday, May 2, 2013

Naibu Waziri awekwa katika wakati mgumu

Naibu Waziri wa Ujenzi, Gerson Lwenge, amegeuka mbogo baada ya mmoja wa wamiliki wa magari ya mizigo kumwambia amewadanganya wabunge kuwa hafahamu ucheleweshaji wa vibali vya magari ya kunyanyulia vitu vizito.

Aidha, Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage, (CCM), aeleza jinsi alivyozomewa na wakazi wa Mkoa wa Morogoro, baada ya watu wawili waliobanwa katika ajali kushindwa kuokolewa kwa sababu ya kukosekana kwa vifaa.

Hali hiyo ilitokea juzi wakati Chama cha Wamiliki wa Magari ya Mizigo (Tatoa), walipokutana na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu pamoja na mawaziri.

Mawaziri waliohudhuria mbali ya Lwenge, ni Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk. Charles Tizeba na Naibu Waziri wa Fedha, Janeth Mbene. Baada ya Tatoa kuelezea kero zao kuhusu sekta ya usafirishaji, mawaziri walipewa nafasi ya kujibu kero hizo na Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Peter Serukamba.

Lwenge alisema suala la rushwa katika mizani ambalo linalalamikiwa na chama hicho linahusu pande mbili yaani mtoaji na mpokeaji. Kuhusu vibali vya magari ya kubebea vitu vizito kuchukua muda mrefu, aliwataka kwenda ofisini kwake kuzungumza naye iwapo kuna tatizo hilo. Wakati akiendelea kuelezea ndipo mmliki huyo aliposimama na kusema kuwa waziri amedanganya hadhara hiyo kwa kuwa wameshapeleka malalamiko hayo kwa maandishi mara kadhaa bila ufumbuzi.

Maneno hayo yalionekana kumkera sana Lwenge na kuja juu akimtaka mmiliki huyo kumsikiliza na yeye. Hata hivyo, Dk. Tizeba aliingilia kwa kusema wao kama serikali wameyasikia na kuwa watakaa na kuyatafutia ufumbuzi wa kero hizo na kisha kuwajibu.

Kuhusu kero ya matuta, Lwenge alielezea kuhusiana na kero ya matuta yaliyowekwa katika barabara, alisema tayari wameshaanza kuondoa matuta yasiyo na viwango ambayo yamekuwa  ni kero kwa wasafirishaji.

Hata hivyo, alikumbana na swali kutoka kwa Serukamba likimtaka atoe
mfano wa barabara ambazo matuta yameondolewa na ndipo alipotaja barabara ya Dar es Salaam kwenda Dodoma.

“Mimi Mheshimiwa waziri nimepita hapo juzi, matuta yapo vile vile,” alisema Serukamba, hali iliyomfanya waziri kubadilisha kauli yake kwa kukiri kuwa hayajaondolewa.

Kuhusu msongamano katika mpaka wa Tunduma, Dk.  Tizeba, alisema ujumbe wa Tatoa na serikali utaondoka kwenda Zambia Mei 7 kujadiliana. Mwijage aliitaka serikali kuchukua hatua ya kununua vifaa vya kuokolea wakati inapotokea ajali. “Nilipita pale nikakuta kuna ajali imetokea  watu wamebanwa na vyuma wameshindwa kuokolewa,  walipogundua kuwa mimi ni mbunge nilizomewa ilikuwa ni aibu,” alisema.

Mbunge mwingine aliitaka serikali kuangalia risiti zinazotolewa bandarini kwa kuwa watu huandikiwa katika vikaratasi wanapotozwa fedha.  Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby (CCM), alishangazwa na hatua ya serikali kuweka mizani mingi njiani wakati gari linapoondoka bandarini linapimwa na kufungwa vizuri.

Pia alikerwa na tabia ya kampuni za udalali ya  Yono na Majembe, ambazo alisema zimekuwa zikiwabughudhi wamiliki wa magari hayo kwa kuyakamata ovyo.

No comments: